MGOMBEA urais wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk John Magufuli amesema
Serikali atakayoiongoza baada ya kuchaguliwa, itapandisha mishahara ya
watumishi wote wa umma ilingane na ile ya Wakala wa Taifa wa Barabara
(Tanroads), ambayo aliianzisha na kuwapa wafanyakazi wake mishahara
minono.
Hata hivyo, Dk Magufuli alisema baada ya kuongeza mishahara hiyo,
wafanyakazi lazima wachape kazi na kuonya kuwa wasipofanya hivyo
atapambana nao. Aidha, amesema Serikali atakayoiongoza, itapunguza bei
ya vifaa vya ujenzi, hasa saruji na mabati.
Alisema hayo jana katika mikutano midogo aliyofanya njiani alikokuwa
akisimamishwa na wananchi wakati alipokuwa akitoka Songea, kupitia
Namtumbo na Tunduru kwenda Masasi mkoani Mtwara.
Dk Magufuli alisema mkoani Mtwara tayari ujenzi umeanza wa kiwanda
cha saruji ambacho ndio kikubwa kuliko vyote Afrika Mashariki na Kati na
kikikamilika, kitazalisha saruji nyingi na kupunguza bei ya bidhaa hiyo
muhimu ya ujenzi.
Alisema kusudio la kushusha bei ya vifaa hivyo ni kusaidia wananchi
wajenge nyumba nzuri na bora za makazi kwa ajili ya kuboresha maisha
yao. Kuhusu kuboresha kipato cha wananchi ili wafanikishe azma ya
kutumia punguzo la bei za bidhaa za ujenzi na kujenga nyumba bora, Dk
Magufuli alisema umeme umeanza kufika katika maeneo hayo na Serikali
yake itahakikisha vijijini kunajengwa viwanda vidogo vitakavyotoa ajira
vijijini.
Mbali na ajira, pia aliahidi kutoa Sh milioni 50 kwa kila kijiji na
kila mtaa, kwa ajili ya kuanzisha na kuendeleza miradi midogo midogo ya
kujipatia kipato kwa ajili ya wanawake na vijana.
Wednesday, 2 September 2015
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 comments:
Post a Comment