YANGA na Azam leo zinakutana kwenye Uwanja wa Taifa Dar es Salaam
katika mechi ya Ngao ya Jamii kuashiria uzinduzi wa Ligi Kuu
inayotarajiwa kuanza kutimua vumbi mwishoni mwa wiki hii.
Timu hizo kwa muda mrefu zimekuwa zikipokezana kijiti kwenye anga za soka la kitaifa na kimataifa ambapo mwaka huu.
Azam ilishiriki michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika na kutolewa
mapema na Yanga iliyokuwa ikishiriki Ligi ya Mabingwa kabla ya kuangukia
kwenye Kombe la Shirikisho ipo hatua ya makundi ya michuano hiyo licha
ya kutokuwa na nafasi ya kusonga mbele.
Mara ya mwisho timu hizo zilikutana kwenye fainali ya Kombe la
Shirikisho la TFF katika Uwanja wa Taifa ambapo Yanga ilishinda mabao
3-1. Aidha Yanga iliendelea kuitambia Azam tena katika mechi ya ngao ya
Jamii msimu uliopita ambapo iliichapa kwa mikwaju ya penalti 8-7 baada
ya kutoka sare ya bila kufungana kwa dakika 120 .
Katika mechi ya leo, Yanga itashuka dimbani ikitoka kupata ushindi wa
bao 1-0 katika mchezo wa Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya Mo Bejaia
Jumamosi iliyopita baada ya kucheza mechi nne mfululizo kwenye michuano
hiyo bila ushindi.
Lakini pia, ikiwa na rekodi ya kupoteza michezo kadhaa iliyopita ya
michuano hiyo dhidi ya TP Mazembe 1-0, Medeama ugenini (3-1) na nyumbani
(1-1), Mo Bejaia ugenini (1-0).
Yanga sasa inasubiri kukamilisha ratiba dhidi ya Mazembe katika mechi
ya mwisho ya makundi baada ya kutokuwa na nafasi ya kufuzu nusu fainali
ya michuano hiyo kutokana na ushindi wa mabao 3-2 wa Medeama dhidi ya
Mazembe mwishoni mwa wiki iliyopita.
Kocha Mkuu wa Yanga Hans Pluijm alisema jana kuwa wamesahau
yaliyopita na matarajio yao ni kushinda mchezo wa leo ili kuwa na mwanzo
mzuri wa maandalizi ya Ligi Kuu Tanzania bara wakiwa mabingwa watetezi.
“Hakuna timu yoyote inayotutisha na kila siku tumekuwa tukifanya
mazoezi na kujiimarisha, lengo letu ni kuendeleza rekodi ya kushinda
mataji,” alisema.
Huenda Yanga ikawakosa wachezaji wake muhimu kama kipa Ally Mustafa
‘Barthez’ anayesumbuliwa na maumivu ya kifundo cha mguu, mabeki Juma
Abdul, Andrew Vincent ‘Dante’ wanaosumbuliwa na maumivu ya miguu, Kevin
Yondani anayeumwa jicho na kiungo Obrey Chirwa anayeumwa goti.
Aidha, mchezo wa leo utakuwa ni mtihani mkubwa wa kwanza kwa Kocha
Mkuu wa Azam Mhispania Zeben Hernandez ambaye aliahidi kurejesha imani
ya mashabiki wa Azam FC kwani anatarajia kutumia mfumo wa pasi nyingi
ambao unatumiwa na timu ya Ligi Kuu Hispania ‘La Liga’ Barcelona.
Timu hiyo imefanya maandalizi ya muda mrefu na kucheza mechi kadhaa
za kirafiki ikiwa ni sehemu ya maandalizi yao ya ligi. Ilicheza dhidi ya
URA ya Uganda (1-1), dhidi ya Friends Rangers (2-1), Ashanti United
(2-0), Mshikamano (1-0), Kombaini ya Wilaya ya Mjini (1-0), Taifa
Jang’ombe (1-0), na sare mbili ilipocheza na JKT Ruvu (1-1) na Ruvu
Shooting (1-1).
Akizungumzia mchezo huo Hernandez, aliweka wazi kuwa ana uhakika
mkubwa wa kuifunga Yanga kwenye mchezo wa leo kwani tayari amepata
kikosi chake cha kwanza baada ya michezo hiyo ya kirafiki.
“Siwezi kuzungumzia sana mechi ya Yanga kwa sababu naamini ya kuwa
jitihada zangu na taaluma ninayowapa wachezaji wangu naamini itatoa
matunda, lakini natambua ya kuwa Yanga ni timu ya zamani ipo na inacheza
vizuri, kikubwa naamini nitashinda mchezo huo kulingana na kile
ninachowapa wachezaji wangu,” alisema.
Azam FC huenda ikawakosa wachezaji wake Aggrey Morris na Paschal Wawa
ambao ni majeruhi wa muda mrefu, ingawa wameshaanza mazoezi mepesi.
Lakini pia, wanajivunia usajili wa beki mpya Bruce Kangwa anayetokea
Highlanders ya Zimbabwe.
Wednesday, 17 August 2016
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 comments:
Post a Comment