KOCHA wa Yanga Hans van der Pluijm, ameitupia lawama safu yake ya
ulinzi kwa kusema ilikosa umakini na kusababisha wapinzani wao Mwadui FC
kusawazisha bao la pili dakika za mwisho.
Yanga juzi ilikuwa ugenini Uwanja wa Kambarage Shinyanga kupambana na
Mwadui FC, na kulazimishwa sare ya 2-2, matokeo ambayo yameiweka rehani
nafasi yake ya kuongoza ligi hiyo.
Akizungumza na gazeti hili Pluijm, alisema safu yake ya ulinzi
iliwanyima pointi tatu kwenye mchezo huo kitu ambacho kinaweza
kuwagharimu kutokana na ushindani mkali uliopo kati yao na wapinzani wao
Azam FC.
“Hatukucheza kwenye kiwango chetu cha kawaida, lakini tulistahili
ushindi kutokana na namna ambavyo wachezaji wangu walivyocheza kwa
kujitolea na kupata mabao yale mawili.
“Hata hivyo safu yetu ya ulinzi ilituangusha kwa kuruhusu bao la
kusawazisha la dakika za mwisho,” alisema Pluijm. Mholanzi huyo alisema
matokeo hayo siyo mabaya, lakini wanalazimika kupambana kwenye mchezo
wao unaokuja dhidi ya Kagera Sugar ili kurudisha wimbi lao la ushindi na
kuendelea kujiwekea mazingira mazuri ya ubingwa msimu huu.
Alisema katika mchezo huo wapinzani wao Mwadui, walionekana kucheza
kwa kutumia nguvu nyingi na kuwakamia, kitu ambacho kiliwasumbua
wachezaji wake kushindwa kuonesha kiwango chao cha kawaida ambacho
wamekuwa wakikionesha kwenye michezo iliyopita.
“Mchezo ulikuwa mgumu kwa sababu tulicheza na timu ambayo ilipania
kutuvurugia mipango yetu kwa kucheza vurugu, lakini nimefurahi kupata
sare hiyo kwa sababu vijana wangu walilazimika kubadilika na kuendana na
hali ya mchezo ilivyokuwa,” alisema Pluijm.
Katika mchezo huo mabao ya Yanga yote mawili yalifungwa na Mzimbabwe
Donald Ngoma, huku yale ya Mwadui yakifungwa na Poul Nonga na Bakari
Kigodeko na kuifanya timu hiyo ya Jangwani kufikisha pointi 20 katika
mechi nane ilizocheza msimu huu.
Friday, 30 October 2015
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 comments:
Post a Comment