DAKTARI wa Kemia, John Pombe Joseph Magufuli ndiye Rais wa Tano wa Tanzania.
Jana ambapo alitimiza miaka 56 ya kuzaliwa kwake, Tume ya Taifa ya
Uchaguzi (NEC) ilimtangaza kuwa mshindi wa Uchaguzi Mkuu wa Urais mwaka
2015, uliofanyika Jumapili iliyopita.
Mbunge huyo wa Chato kwa miaka 20, aliyezaliwa Oktoba 29, 1959,
ametangazwa mshindi baada ya kupata kura 8,882,935, sawa na asilimia
58.46 ya kura halali zilizopigwa Jumapili, hivyo kumrithi Rais Jakaya
Kikwete katika Ikulu ya Magogoni ambayo tayari imeshakaliwa na
Watanzania wengine wanne.
Mbali ya Rais Kikwete, marais wengine waliowahi kuiongoza Tanzania ni
Mwalimu Julius Nyerere, Ali Hassan Mwinyi na Benjamin Mkapa, ambao
wameshika madaraka hayo ya juu ya nchi tangu Uhuru wa mwaka 1961.
Akitangaza matokeo hayo jana kwenye Ukumbi wa Kimataifa wa Mwalimu
Julius Nyerere (JNCC), Dar es Salaam, Mwenyekiti wa NEC, Jaji mstaafu
Damian Lubuva alisema Dk Magufuli ameshinda nafasi hiyo baada ya
kujikusanyia kura 8,882,935 ambayo sawa na asilimia 58.46 ya kura halali
zilizopigwa.
“Kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya mwaka 1977 Ibara ya
41 (6) mgombea yeyote wa kiti cha urais atatangazwa kuwa amechaguliwa
kuwa rais, iwapo tu amepata kura nyingi zaidi kuliko mgombea mwingine
yeyote. Na Ibara ya 47 (ii) inasema mgombea urais akichaguliwa kuwa
mshindi, basi mgombea mwenza atatangazwa kuwa Makamu wa Rais,” alisema
Jaji Lubuva.
“Kwa mujibu wa Sheria ya Uchaguzi Kifungu wa 35 (e) na 35 (f) na
Kifungu cha 81 (b) vya Sheria ya Uchaguzi Sura ya 343, namtangaza John
Magufuli kuwa mshindi wa uchaguzi wa Rais wa mwaka 2015 na pia
namtangaza Samia Suluhu Hassan kuwa Makamu wa Rais.” Kwa msingi huo,
Mgombea Mwenza wa CCM, Samia Suluhu Hassan atakuwa Makamu wa Rais, akiwa
ni mwanamke wa kwanza kushika wadhifa huo Tanzania tangu nchi
ilipoundwa.
Dk Magufuli alifuatiwa na mgombea wa Chama cha Demokrasia na
Maendeleo (Chadema) aliyeungwa mkono na vyama vinne vya upinzani
(Ukawa), Edward Lowassa aliyepata kura 6,072,848, sawa na asilimia 39.97
ya kura halali zilizopigwa.
Kwa mujibu wa Mkurugenzi wa Uchaguzi, Kailima Kombwey, katika
uchaguzi wa mwaka huu, wapiga kura 23,161,440 walijiandikisha na
waliopiga kura ni 15,589,639, ambayo ni asilimia 67.31 ya
waliojiandikisha.
Kombwey alisema kura halali ni 15,193,862 ambayo ni asilimia 97.46 na
kura zilizokataliwa ni 402,248 ambayo ni asilimia 2.58. Katika uchaguzi
huo, ambao wagombea wa urais walikuwa wanane, mwanamke pekee, Anna
Mgwhira wa chama kipya cha ACT-Wazalendo alishika nafasi ya tatu kwa
kupata kura 98,763 sawa na asilimia 0.65.
Wagombea wengine kura walizopata na asilimia kwenye mabano ni Chief
Lutalosa Yemba wa ADC kura 66,049 (asilimia 0.43), Hashim Rungwe wa
Chaumma kura 49,256 (asilimia 0.32), Janken Kasambala wa NRA kura 8,028
(asilimia 0.05), Macmillan Lyimo wa TLP kura 8,198 (asilimia 0.05),
Fahmi Dovutwa wa UPDP kura 7,785 (0.05%).
Katika uchaguzi uliofanyika mwaka 2010, mgombea wa CCM, Jakaya
Kikwete alishinda uchaguzi huo akiwa amepata asilimia 61.17 baada ya
kupata kura zaidi ya milioni 5.27 na kufuatiwa na mgombea wa Chadema, Dk
Willbrod Slaa aliyepata kura ya zaidi ya milioni 2.27.
Nafasi ya tatu ilikwenda kwa Profesa Ibrahim Lipumba wa CUF aliyepata
kura 697,014, Peter Mziray alipata kura 96,932, Rungwe aliyegombea kwa
tiketi ya NCCRMageuzi alipata kura 26,321, Mutamwega Mughwaya wa TLP
alipata kura 17,434 na Dovutwa alipata kura 13,123. Ujumlishwaji wa
matokeo ulishuhudiwa na mawakala wa vyama mbalimbali, waangalizi, Polisi
pamoja na wananchi wa kawaida, pamoja na kuhakiki matokeo hayo.
Hata hivyo, vyama viwili kati ya vinane vilivyoshiriki uchaguzi
havikusaini matokeo hayo ambavyo ni Chadema na Chaumma. Chadema katika
majumuisho, wakala wake Goodluck ole Medeye, waziri wa zamani katika
Serikali ya Awamu ya Nne aliyemfuata swahiba wake Lowassa katika
Chadema, ambaye alikuwepo wakati wa kutangaza matokeo ya majimbo,
hakuwepo wakati wa kujumuisha na kusaini matokeo huku wakala wa Chaumma
akigoma kusaini.
Mkurugenzi wa Uchaguzi wa NEC, Kailima Kombwey alisema pamoja na
mawakala hao kugoma kusaini hakuzuii, Tume kutangaza matokeo ya
uchaguzi. Kwa mujibu wa Kombwey, Rais mteule Dk Magufuli atakabidhiwa
cheti cha ushindi leo kwenye Viwanja vya Diamond Jubilee, Dar es Salaam
pamoja na Makamu wa Rais, Samia.
Dakika chache kabla ya Dk Magufuli kutangazwa na NEC baada ya
kumaliza kujumuisha matokeo, ambayo yalianza kutangazwa kwa umma kuanzia
Jumatatu asubuhi, Rais Kikwete aliweka picha ya Magufuli katika akaunti
yake ya Twitter na kuandika, “Amiri Jeshi Mkuu mpya wa Tanzania, chaguo
la Watanzania, Rais John Pombe Magufuli.”
Aidha, mgombea wa ACT – Wazalendo, Anna Mghwira alimpigia simu Dk
Magufuli muda mfupi baada ya kutangazwa mshindi na kumpongeza, huku Dk
Magufuli akimshukuru na kumwita mkomavu wa siasa na mwanademokrasia wa
mfano.
Kwa mujibu wa Rais Kikwete, baada ya kupiga kura kijijini kwake Msoga
wilayani Bagamoyo, ataondoka madarakani kwa mujibu wa Katiba Alhamisi
ya Novemba 5, mwaka huu, siku ambayo Dk Magufuli atakula kiapo kwenye
Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam kuiongoza Tanzania kwa miaka mitano
ijayo.
Dk Magufuli ambaye ni Waziri wa Ujenzi, atakuwa Rais wa kwanza wa
Tanzania ambaye ni mwanasayansi, na pia mwalimu wa tatu kukaa Ikulu ya
Magogoni, akitanguliwa na walimu wenzake Mwalimu Nyerere na Alhaj
Mwinyi.
Amewahi kufundisha katika Shule ya Sekondari ya Sengerema mkoani
Mwanza akifundisha masomo ya Kemia na Hisabati, na baadaye kufanya kazi
katika Chama cha Ushirika cha Nyanza jijini Mwanza akiwa Mkemia.
Alijitosa katika siasa ambako alichaguliwa kuwa Mbunge wa Jimbo la
Biharamulo Mashariki mkoani Kagera (wakati huo sasa Chato mkoani Geita)
mwaka 1995. Amekuwa mbunge wa jimbo hilo hadi Juni mwaka huu,
alipojitosa katika mchakato wa kuwania urais. Aliteuliwa na Rais Mkapa
kuwa Naibu Waziri wa Ujenzi kuanzia mwaka 2000 hadi mwaka 2005. Baadaye
alikuwa Waziri kamili wa wizara hiyo.
Chini ya Rais Kikwete, amewahi kuwa Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na
Uvuvi, Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, kabla ya kumrejesha Ujenzi.
Dk Magufuli anasifika kwa uchapakazi na weledi katika kazi zote,
alizokabidhiwa akiwa serikalini na wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu
kaulimbiu yake ilikuwa “Hapa Kazi Tu”.
Kaulimbiu hiyo ilimbeba na kumpambanua na wagombea wengine saba, huku
akiahidi kuwa Tanzania itakuwa nchi ya viwanda chini ya uongozi wake.
Katika uchaguzi uliokuwa na ushindani mkubwa pengine kuliko chaguzi
nyingine nne za mfumo wa vyama vingi ulioanzishwa mwaka 1992, Dk
Magufuli aliendesha kampeni zake, akijipambanua kuwa ni mtu atakayeleta
mabadiliko ya kweli katika utendaji wa serikali.
Aliwaahidi Watanzania kwamba atasimamia mabadiliko hayo katika kila
sekta, akisisitiza zaidi maendeleo ya viwanda hasa katika kuiwezesha
Tanzania kuingia kuwa nchi ya uchumi wa kati.
Akifunga kampeni zake jijini Mwanza kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Dk
Magufuli alisema amepokea ushauri kutoka kwa wananchi kwa njia
mbalimbali, kutoka facebook, tweeter, mabango, vikao mbalimbali na hata
ujumbe mfupi wa simu ambapo alisema imeonekana kero kubwa ni maji.
Kero nyingine alizoahidi kushughulikia ni ya nishati ya umeme,
kulinda Muungano, kuendeleza ulinzi na usalama wa nchi na wananchi wake,
kuimarisha kilimo, uvuvi na ufugaji kwa kuboresha bei ya mazao ya kazi
hizo na kuimarisha viwanda, viongeze thamani ya mazao hayo.
Aliahidi kuhakikisha kila Mtanzania mwenye uwezo wa kufanya kazi
anapata kazi yenye kipato kizuri, kutoa mikopo ya Sh milioni 50 kila
kijiji na mtaa ya kuanzisha na kuendeleza biashara, kuhakikisha elimu
inatolewa bure kuanzia awali mpaka kidato cha nne na kuwashughulikia
mafisadi kwa kuanzisha Mahakama ya Rushwa.
Mshindani wake wa karibu, Waziri Mkuu wa zamani, Lowassa ambaye
alikuwa ndani ya CCM kabla ya kujitoa Agosti mwaka huu, aliingia Chadema
na kubeba kaulimbiu ya mabadiliko, huku akiwaahidi Watanzania kuwa
ataendesha serikali kwa mchakamchaka na kubadili hali ya maisha kwa
Watanzania kwa muda mfupi.
Friday, 30 October 2015
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 comments:
Post a Comment