AZAM FC jana iliweka historia kwa kutwaa kwa mara ya kwanza taji la
Kagame baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Gor Mahia ya
Kenya katika fainali iliyopigwa kwenye Uwanja wa Taifa Dar es Salaam.
Ubingwa huo wa Azam FC umemaliza ubabe wa Yanga na Simba kwa Tanzania
kutwaa taji hilo, ambalo limechukuliwa na wekundu wa Msimbazi mara sita
huku vijana wa Jangwani wakilitwaa mara tano.
Mbali na kumaliza ubabe wa vigogo hivyo, Azam FC pia imeweka historia
nyingine baada ya kumaliza mashindano hayo bila ya kufungwa bao hata
moja kuanzia mwanzo wa mashindano hayo hadi mwisho.
Pia, Azam imemaliza ukame wa taji hilo ililonusurika kulitwaa mwaka
2012 ilipofungwa na Yanga 2-0 katika fainali iliyofanyika kwenye Uwanja
wa Taifa. Katika mchezo huo, Azam FC ndio walikuwa wa kwanza kulifikia
lango la Gor Mahia mara mbili mwanzoni kabisa mwa mchezo, kabla
wapinzani wao hawajajibu wakati Medieval Kagere alipotaka kufunga.
Dakika ya 15 John Bocco aliipatia Azam bao la kwanza akimalizia krosi
ya Kipre Tchetche. Muda mfupi kabla ya mapumziko, Azam FC ilionekana
kupungukia nguvu na kuifanya Gor Mahia kufanya mashambulizi ya mara kwa
mara katika lango la wapinzani wake hao.
Dakika ya 51 Azam nusura wapige bao la pili baada ya Tchetche kupiga
shuti kali lililogonga mwamba wa pembeni na mpira kurudi uwanjani kabla
haojaokolewa. Juhudi za Azam zilizaa matunda wakati Tchetche alipoipatia
timu yake bao la pili baada ya kupiga mpira wa adhabu uliokwenda moja
kwa moja wavuni ukimuacha kipa wa Gor Mahia Boniface Oluoch akidua bila
la kufanya.
Mwamuzi alitoa adhabu hiyo baada ya Shomari Kapombe kuchezewa rafu na
Aucho Khalid aliyeoneshwa kadi ya njano kwa mchezo huo mbaya. Azam FC
wangeweza kufunga la tatu kama sio kukosa umakini kwa mchezaji wake,
Didier Kavumbagu baada ya kukosa bao la wazi katika dakika ya 90 wakati
alipopaisha mpira.
Vikosi: Azam FC: Aishi Manula, John Bocco, Aggrey Morris, Said Morad,
Pascal Wawa, Jean Mugiraneza, Humid Mao, Farid Mussa/ Erasto Nyoni,
Amme Ali/Frank Domayo, Shomari Kapombe na Kipre Tchetche. Gor Mahia:
Boniface Oluoch, Mussa Mohamed, Sibomana Abouba, Harun Shakava, Karim
Nizigayamana, Innocent Wafula, Such Khalid, Godfrey Walusimbi, Kagere
Medie, Michael Olunga na Erick Ochieng.
Sunday, 2 August 2015
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 comments:
Post a Comment