.

.

Wednesday, 3 June 2015

Waziri Mkuu mstaafu, Frederick SumayeWaziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye
MAKADA wa CCM waliotangaza nia ya kuwania urais, sasa wamefikia tisa baada ya jana Profesa Sospeter Muhongo, Frederick Sumaye na Dk Titus Kamani, kutangaza rasmi dhamira hiyo wakiwa katika miji mitatu tofauti nchini.
Sumaye, Waziri Mkuu mstaafu alitangaza nia akiwa Dar es Salaam, Profesa Muhongo, Waziri wa Nishati na Madini aliyejiuzulu hivi karibuni alitangaza akiwa Musoma wakati Dk.
Kamani ambaye ni Waziri wa Maendeleo na Mifugo na Uvuvi alitangaza nia akiwa Mwanza.
Wengine waliokwishatangaza ni Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, Waziri wa Kilimo, Chakula la Ushirika, Stephen Wassira, Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalumu) Profesa Mark Mwandosya, Mbunge wa Afrika Mashariki, Charles Makongoro Nyerere na Balozi mstaafu, Ali Karume.
Sumaye na rushwa, ufisadi Sumaye, akitangaza rasmi nia yake jijini Dar es Salaam, alisema endapo atapatiwa ridhaa na chama chake pamoja na Watanzania atapambana kwa hali na mali kuondoa tatizo la rushwa na ufisadi.
Sumaye aliyeshika nyadhifa mbalimbali serikalini ikiwa ni pamoja na uwaziri mkuu kwa miaka 10, alisisitiza kuwa ametangaza nia hiyo kwa kuwa tayari ameshapima, ametafakari na kujiridhisha kuwa anatosha kuwaongoza Watanzania.
“Mimi naweka wazi leo hii, tatizo la ufisadi na rushwa kwangu halivumiliki kwanza nayachukia kabisa matendo hayo. Nawahakikishia Watanzania mkinipa ridhaa nipatambana na rushwa na ufisadi kwa ujasiri bila uoga wowote, nitawashughulikia wote watakaohusika bila kujali sura, vyeo, urafiki wala nafasi zao katika nchi hii,” alisisitiza.
Alisema amewasikia baadhi ya wagombea wenzake wa nafasi ya urais ndani ya CCM, kila mmoja kwa wakati wake akizungumzia kupambana na rushwa.
Aliongeza kuwa “Kuna mmoja wao anasema eti Watanzania hawataki kiongozi masikini kwa hiyo huyu kwa namna nyingine anataka kiongozi tajiri, cha kushangaza mtu huyo anasema yeye si tajiri bado anatafuta utajiri, tena anataka urais, sasa swali hivi Ikulu ndiko kwenye utajiri?” Alihoji Sumaye.
Akizungumzia sababu za kutaka kuwania urais, Sumaye aliyejaribu urais mwaka 2010, alisema pamoja na kujipima na kuona anatosha, Watanzania wengi wanamtambua kutokana na kuwa kiongozi wa muda mrefu ambaye alitumikia Serikali ya awamu ya tatu kwa uadilifu na mafanikio makubwa.
“Tangu mwaka 1985 nimekuwa mbunge, nimekuwa Naibu Waziri, nikawa Waziri, na baadaye Waziri Mkuu kwa miaka 10 mfululizo, kwa hiyo kama ni jeshini mimi ni yule unayeweza kusema mwanajeshi aliyeiva na si kuchupia,” alisisitiza.
Akizungumzia suala la ubinafsishaji wa mashirika ya umma na uuzwaji wa nyumba za Serikali, Sumaye alisema Serikali yake ilitekeleza mipango hiyo kutokana na Sera iliyokuwepo ambayo ilipitiwa na kujadiliwa na Baraza la Mawaziri na Rais kushauriwa.
Aidha, alizungumzia kashfa za benki ya NBC, Rada, Mgodi wa Kiwira, ndege ya Rais zilizoikumba Serikali yake na kubainisha kuwa katika maeneo yote tajwa, hakuna hata moja lenye sifa ya kashfa kwa kuwa yalibinafsishwa kwa taratibu zilizotakiwa huku mengine yakiwa na hali mbaya.
“Tena Kiwira ndio ilikuwa na hali mbaya tangu zamani, bahati mbaya tu akina Daniel Yona na Rais Benjamin Mkapa waliwekeza, kutokana na hali yake Rais Mkapa alijitoa baada ya siku tatu tu,” alisema.
Alisema endapo atapewa ridhaa na chama chake na Watanzania, vipaumbele vyake vitakuwa ni uchumi, rushwa, huduma za jamii, muungano, umoja na amani. Katika rushwa ataunda Mahakama maalumu ya kusimamia na kushughulikia kesi za rushwa na ufisadi.
Sumaye alisisitiza kuwa endapo chama hicho kitateua mgombea anayependa rushwa au fisadi, msimamo wake ni kujitoa kwenye chama hicho.
“Ila sijajiandaa kujitoa, kwa kuwa najua chama changu chenye viongozi wengi makini, hakitoweza kamwe kuteua mgombea mwenye sifa mbaya ya ufisadi na rushwa,” alisema.
Muhongo na uchumi Profesa Muhongo amewaomba wana CCM na Watanzania ridhaa ya kugombea urais Oktoba, akisema ana uwezo wa kupaisha uchumi kwa kutumia rasilimali zilizopo, hivyo kumaliza umasikini.
Aliomba ridhaa hiyo jana katika Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT) wilayani Musoma mkoani Mara, na kueleza kuwa atatenga bajeti ya kutosha kwa ajili ya utafiti, ili ukuzaji uchumi na ushindani usifanywe kwa kubahatisha.
Katika maelezo aliyoyatoa kuanzia saa 10:00 jioni, Muhongo alisema kupitia mapinduzi atakayoyafanya katika sekta za elimu, viwanda, kilimo, ufugaji, uvuvi, gesi na madini, kwa kuzingatia utafiti zaidi, atasababisha kukua kwa ajira na pato la taifa, kufikia zaidi ya Dola za Marekani bilioni 200, baada ya miaka 10 kuanzia atakapokuwa Rais.
Muhongo aliyekataa kuahidi chochote kuhusu mishahara ya watumishi wa umma, na ujenzi wa shule, hadi aimarishe uchumi kwa kuiacha nchi ya Kenya mbali, alisema; “Nitahakikisha gesi tuliyonayo inatuletea manufaa katika viwanda na kuianzishia mfuko maalumu ili fedha zake zisiende Hazina, kutoa fursa kwa wakulima, wafugaji, wavuvi na wazalishaji wengine nchini, kukopeshwa mitaji kwa asilimia mbili”.
Mbali na vipaumbele vya utafiti na mapinduzi katika sekta ya gesi, Profesa Muhongo alitaja vingine kuwa ni elimu, aliyoeleza kwamba ataiongezea bajeti na kuboresha maslahi ya walimu na kuwalipa mishahara sawa na madaktari, kama wafanyavyo Finland, kuongeza vifaa vya elimu na kupunguza idadi ya wanafunzi darasani kuwa kati ya 15-35.
Akitoa ufafanuzi wa jinsi atakavyotekeleza vipaumbele vyake na kukuza uchumi, Professa Muhongo alisema, atatumia utaalamu na wataalamu waliopo na atakao waongeza kuhakikisha gesi inaleta mtaji wa Sh bilioni 500 na kuchangia kuzalisha umeme mwingi zaidi.
“Tumegundua gesi kiasi cha futi za ujazo trilioni 56, sawa na mapipa bilioni 10 ya mafuta, yanayoweza kutuletea fedha hizo, hivyo kutuweka katika nafasi nzuri ya kukuza uchumi wa nchi,” alisema.
Kamani na rasilimali za nchi Dk Kamani aliainisha vipaumbele sita muhimu, alivyodhamiria kuvitekeleza katika Serikali yake, endapo atafanikiwa kuingia madarakani, akisema atajikita katika kuimarisha mshikamano wa uongozi unaoshirikisha wananchi katika matumizi ya rasilimali za taifa.
Vipaumbele vyake vingine ni uadilifu kwa taifa, ili kuwawezesha viongozi wa ngazi zote kufanya kazi kwa uadilifu, elimu kwa wote, kuweka mazingira bora ya ajira serikalini na katika sekta binafsi, kuimarisha huduma za afya kwa wananchi wote bila ya kubagua dini, kabila wala rangi zao na kuhakikisha kuwa rasilimali ya nishati, inawanufaisha watu wote na kuhakikisha nchi inakuwa na miundombinu imara muda wote.
Alisema katika uongozi wake, atadhamiria kuijenga Tanzania moja, yenye upendo, amani na mshikamano, uadilifu lakini yenye kuwajali watu wake bila ya kubagua, huku wakiwa na urari sawia wa kumiliki rasilimali za nchi.
Katika kuwa na uhakika wa rasilimali fedha, alisema serikali yake itajiweka mazingira mazuri ya ukusanyaji wa maduhuri ya serikali kwa kuangalia upya vipaumbele vya ujenzi wa uchumi wa taifa, huku akiapa kushughulikia wazembe na wala rushwa.
“Bila ya kudhibiti rushwa taifa litaangamia, nitakuwa mkali katika swala la rushwa”, alisema.
Imeandikwa na Halima Mlacha na Namsembaeli Mduma (Dar), Nashon Kennedy (Mwanza) na Ahmed Makongo (Musoma).

0 comments:

Post a Comment